SERIKALI imetakiwa kutoa mwongozo haraka juu ya mamlaka yenye uamuzi wa matumizi ya fedha za maendeleo ya Sekondari za kata ili kuondoa utata uliopo hivi sasa.
Wito huo umetolewa na baadhi ya madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Iramba wakati wakijadili taarifa ya maendeleo ya elimu kwenye kikao cha baraza kilichofanyika mjini Kiomboi.
Madiwani hao wamesema baada ya Sekondari hizo kurudishwa kwa halmashauri kwa ajili ya usimamizi, hakuna mwongozo juu ya mamna ya kutumia ruzuku inayotolewa na serikali hali inayotoa mwanya mkubwa kwa wakuu wa shule hizo kufanya watakavyo wao.
Kutokana na hali hiyo madiwani hao wamesema kuna haja kwa serikali kuhakikisha kuwa inatoa haraka mwongozo juu ya utaratibu wa matumizi ya fedha za Sekondari hizo.
Wamesema kitendo cha kuendelea kuchelewa kinaweza kusababisha fedha nyingi zikaishia kwenye midomo ya wajanja wachache badala ya kufanya kazi iliyokusudiwa.
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Iramba bw Fortunatus Fwema amewataka madiwani kuwa na subira kwa madai kuwa tayari kuna maelekezo maalum yaliyoanza kutolewa na serikali juu ya namna ya uendeshaji wa shule za Sekondari za kata.
Shule za Sekondari za kata awali zilikuwa zinasimamiwa moja kwa moja na wizara ya elimu kabla ya kukabidhiwa kwa halmashauri na kuteuliwa kwa maafisa elimu kwa ajili ya shughuli hiyo.
.
Radio Free Africa, all rights reserved 1995 - 2009
Na Emmanuel Michael , Singida